Zao la misitu limeonekana kuchangia pato la Taifa kwa asilimia Tatu na kuboresha maisha ya wakazi wanaozunguka zao hilo.
Wilaya ya Mufundi ni moja ya wilaya katika mkoa wa Iringa ambayo kwa asilimia kubwa inajihusisha na kilimo cha Misitu.
Wakazi katika eneo hilo wanazidi kupata umuhimu wa kulima kilimo cha miti baada ya wakuona watu wanaojihusha na zao hilo wananufaika kwa kuuza miti na mbao. Kwa kiasi kikubwa uchumi wa watu wa Wilaya ya Mufindi unategemea zaidi kilimobiashara.
Bwana Tweve ni mkulima wa zao la miti na mkazi wa kata ya Kiholela ambaye anamiliki ekari 70 za miti anasema kilimo cha Miti, ndio kilimo pekee cha mazao ambacho kinainua wakulima wadogo na kukuza uchumi wa taifa kwa kuuza miti hiyo.
"Zao la miti limebadilisha sana maisha yetu binafsi hapa Mufindi, na kaya kwa kuuza miti tu " Anasema Bwana Tweve.
Anasema kilimo hiki, kimesaidia kuboresha hali ya maisha kwa kuwawezesha kujenga nyumba nzuri, kusomesha watoto na kununua vyombo vya moto ili kusafirisha bidhaa muhimu kutoka sehemu moja kwenda nyingine.
Kwa muktadha huo, anatoa wito kwa serikali kurasimisha zao hilo kutumika kama dhamana kwenye taasisi za kifedha ili kuwawezesha kukopa na kukuza zaidi mashamba yao na kupata masoko makubwa ya Kimataifa.