Katika kipindi cha mwezi Aprili hadi kufikia Agosti 3, 2021 Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limekusanya takribani Shilingi Bilioni 3.9 katika zoezi la ukaguzi wa magari bandarini yanayotoka nje ya nchi na kuokoa kiasi cha shilingi Bilioni 2.7 ambayo mwanzo ilikuwa inabaki nje kabla ya zoezi hilo kuanza kufanyika hapa nchini.
Waziri wa Viwanda na Biashara Prof.Kitila Mkumbo ameyasema hayo mara baada ya kutembelea bandari katika kitengo cha kukagua magari zoezi ambalo linafanywa na TBS na kujionea shughuli hiyo ikifanyika.
Amesema mpaka kufikia Agosti 3, 2021 TBS ilifanikiwa kukagua magari 11079 na katika magari hayo 7700 yalikuwa yamekidhi ubora na magari yaliyobaki yalikwenda kutengenezwa na baada ya kutengenezwa magari 1890 yaliweza kukidhi ubora na mengine yaliyobaki yapo gereji yakiendelea kurekebishwa.
“Kwa kuamua kutekeleza mpango huu, Serikali inaokoa fedha nyingi ambazo zingebaki nje hivyo kwa kipindi cha miezi mitatu tumekusanya takribani Bilioni 3.9 na fedha hii inaingia katika mfuko mkuu wa Serikali”. Amesema Prof.Mkumbo.
Awali ukaguzi wa magari kwa kiasi kikubwa ulikuwa unafanyika nje ya nchi na Serikali ilikuwa ikipata asilimia 30% tu za fedha na asilimia 70% zilibaki nje.