KAMPUNI ya mbolea ya Yara Tanzania imejipanga kuwasaidia wakulima wadogo zaidi ya 83,000 kwa kuwapatia mbolea bure.
Lengo la kampuni hiyo ni kuongeza uzalishaji katika kilimo cha mpunga na mahindi nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Winston Odhiambo, alisema zaidi ya tani 12,500 za mbolea ya Yara Mila Cereal yenye thamani ya Sh bilioni 16.5 itagawiwa bure kwa wakulima wadogo maeneo mbalimbali nchini.
“Uzinduzi wa mpango huo unaojulikana kama ‘Action Africa’ utafanywa Alhamisi (kesho) na Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga,” alisema.
Odhiambo alisema Yara Tanzania ambayo ni kampuni tanzu ya Yara International ASA ya Norway, ni mdau muhimu katika maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.
Alisema chini ya mpango huo, mkulima atahitajika kujisajili kupitia namba *149*46*16# kwa kutumia kitambulisho cha mpiga kura au cha taifa na kisha kuzawadiwa mbolea.
“Mpango huu utawasaidia wakulima wadogo wa mahindi na mpunga kuongeza uzalishaji wa mazao hayo na kuondokana na tatizo la njaa,” alisema.