KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imebaini changamoto za mifumo ya kodi katika Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Japhet Hasunga alisema hayo bungeni Dodoma jana wakati akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo kuhusu ripoti za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zilizokaguliwa za serikali kuu na mashirika ya umma kwa mwaka ulioishia Juni 30, mwaka jana.
Hasunga alisema kamati ilipitia na kuchambua taarifa ya hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2022. Hasunga alisema taarifa ya bajeti na makusanyo halisi ya TRA kwa mwaka huo imebainisha kwamba walipangiwa kukusanya Sh trilioni 22.19 lakini makusanyo halisi yalikuwa Sh trilioni 21.3 ikiwa ni pungufu ya Sh bilioni 887.3 sawa na asilimia nne.