Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

JPM, sekta binafsi kuungana kupaisha uchumi

4ece6eb7a772b75c9907b37865ca3295 JPM, sekta binafsi kuungana kupaisha uchumi

Mon, 19 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

RAIS John Magufuli amesema serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), imejipanga kwa kushirikisha sekta binafsi katika kujenga uchumi na kuifanya Tanzania kuwa nchi inayojitegemea kiuchumi.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan aliyasema hayo jana kwa niaba ya Rais Magufuli katika mkutano wa sekta binafsi kumpongeza kiongozi huyo kwa mafanikio ya miaka mitano wakati wa uongozi wake.

Alisema mkutano huo unaipa serikali faraja kutokana na kazi kubwa iliyofanya ndani ya miaka hiyo mitano na matunda yaliyopatikana.

“Kwa ujumla serikali imejipanga na sisi CCM pamoja na serikali zetu mbili Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tunatambua umuhimu wa kujenga uchumi wa kitaifa, ili kuhakikisha Watanzania ndio wanaofaidika na uchumi na rasilimali za nchi,” alisema.

Samia alisema serikali inatambua sekta binafsi ndio itakayofanyakazi kubwa ya kujenga uchumi wa Tanzania na kuwa na sauti ya namna ya kutumia rasilimali za nchi.

“Tunapokwenda tunaweka mazingira kwamba sekta binafsi ndio tutakaokaa nao juu ya meza kupanga namna ya kutekeleza mambo yetu,”alisema Samia na kuongeza;

“Kauli yenu tunaitambua na kauli yenu ndio itakayoendesha uchumi wa nchi hii. Tunatambua nafasi ya sekta binafsi katika kujenga uchumi wa taifa wa kiushindani. Na ilani ya CCM ndio inavyozungumza,”alisema.

Alisema serikali endapo itarejea madarakani itahakikisha sekta binafsi inalindwa na kuendelezwa, haki ya kila mtu, kikundi na ushirika wa kuendesha shughuli za kibiashara vinalindwa wakati wote.

“Tutalinda mazingira ya biashara na kukuza uchumi kwa kuhakikisha tunadumisha amani na usalama na utawala wa sheria, pia tutalinda utulivu ndani ya nchi, siasa zenye heshima na utulivu ili kutoa fursa kwa uchumi kukua. Pia tunaweka ubora wa miundombinu, uchukuzi, nishati na mawasiliano,” alieleza.

Alibainisha kuwa wamejipanga kupunguza gharama za kufanya biashara nchini na kuweka utulivu wa uchumi na biashara ili kuhakikisha mambo yanatabirika na kwenda mbele.

“Pia tutahakikisha kuwa na urahisi, ufanisi wa sheria, kanuni na taratibu,”.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) Angella Kairuki alisema mkutano huo una kongani 14 kutoka sekta binafsi.

Alisema kupitia ofisi ya waziri mkuu uwekezaji, wanaendelea na maboresho ya sera ya uwekezaji ambapo TPSF pamoja na wanachama wake wamekuwa na mchango mkubwa katika kutoa maoni yao yatakayosaidia kupatikana kwa sera na sheria iliyo bora.

“Pia tunaendelea kutekeleza mpango wa biashara na uwekezaji kupitia road map ambapo tozo zaidi ya 228 zimefutwa ndani ya miaka mitatu,” alieleza.

Alisema wizara hiyo imeshirikiana pia na TPSF kuandaa mfumo mahsusi kwa ajili ya kutatua changamoto mbalimbali ambao uko tayari ambao unakusudiwa kuanzia mwakani hadi mwaka 2022 utaanza kupokea kero na maoni mbalimbali.

Chanzo: habarileo.co.tz