Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Jumanne Shauri amesema kuanzia leo Jumatatu hadi Juni 30, Halmashauri hiyo imeanza operesheni ya kuhakikisha wafanyabiashara wasiokuwa na leseni za biashara wanakata leseni hizo ili wafanye shughuli zao kwa ufanisi.
Amesema ikifika Julai Mosi operesheni hiyo itaambatana na wafanyabiashara wasiokuwa na leseni kukata leseni pamoja na faini inayoanzia Sh 100,000 hadi Sh1milioni.
Shauri ametoa kauli hiyo, leo Jumatatu Juni 17, 2019 wakati akizungumza na wanahabari kuhusu ukusanyaji wa mapato ya halmashauri hiyo kuanzia Julai mwaka jana hadi Mei, mwaka huu.
Amesema wamefanikiwa kukusanya Sh52 bilioni kati ya Sh56bilioni walizopanga kuzikusanya.
Amesema wana upungufu wa Sh2bilioni na eneo ambalo hawajafanya vizuri kwenye ukusanyaji wa mapato ni la leseni za biashara hasa kwa wafanyabiashara biashara wa Kariakoo na Kata ya Jangwani.
“Asilimia kubwa eneo lililoturudisha nyuma ni leseni za biashara, zipo zaidi ya leseni 33,000 lakini waliokata leseni ni takriban 23,000. Karibu wafanyabiashara 10,000 bado hawana leseni ndiyo maana tumeamua kufanya operesheni hii itakayosaidia kupata Sh2bilioni ili kufikia lengo la bajeti,” amesema Shauri.
Pia Soma
- Mwigulu ataka ‘Mwigulu staili’ itambuliwe kama vazi rasmi la Taifa
- Zuio la plastiki neema kwa wanawake Pangani