Hatimaye vituo 26 vya mafuta vilivyofungiwa katikati ya Agosti mwaka huu vikidaiwa kutoweka vinasaba kwenye mafuta vimefunguliwa.
Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati Tanzania (Ewura) ilisitisha vituo hivyo kufanya kazi baada ya kubainika kukiuka maelekezo ya kuweka vinasaba kwenye mafuta kama inavyotakiwa kwa mujibu wa sheria.
Ewura kwa kushirikiana na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) wamesema baadhi ya vituo vya mafuta vinavyomilikiwa na kampuni sita za mafuta vimekiuka maelekezo hayo, hatua ambayo imetafsiriwa kama ukwepaji wa kodi.
Kulingana na sheria, mafuta ambayo hayaweki vinasaba ni yale yanayokwenda nje ya nchi na yanayotumika kwenye miradi mikubwa hivyo hupata msamaha wa kodi.
Meneja Uhusiano wa Umma na Mawasiliano wa Ewura, Titus Kaguo amesema kampuni hizo tayari zimefanyia kazi dosari hiyo hivyo vituo vyake vinaweza kufunguliwa tu baada ya kulipa faini na ushuru uliodaiwa na TRA.
Ili vituo hivyo kurejesha huduma zake walitakiwa kulipa faini ya Sh milioni 7 kila kimoja sawa na Sh182 milioni pamoja na kodi ya TRA.