Dar es Salaam. Mkaguzi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Ilala, Mtarazuki Saburi amesema huenda chanzo cha moto unaoteketeza Hoteli ya White Sands iliyopo ufukweni mwa bahari ya Hindi ni hitilafu ya umeme.
Akizungumza na MCL Digital, Saburi amesema walipofika katika hoteli hiyo iliyoanza kuwaka moto leo Ijumaa Agosti 31, 2018 saa 10 jioni, walikuta umesambaa eneo kubwa.
Amesema katika jitihada za kuzima moto huo wamekumbana na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na pampu za kuvuta maji kutoka katika mabwawa ya kuogelea kushindwa kuvuta maji ipasavyo.
Saburi amesema kuwa wateja waliokuwa katika hoteli hiyo wamehamishiwa maeneo mengine, huku uongozi wa hoteli hiyo ukisema utatoa taarifa rasmi kesho.