Kukatika kwa huduma ya Facebook, Instagram na WhatsApp zinazomilikiwa na Mark Zuckerberg, Jumatatu ya wiki, kumeathiri vibaya biashara za watu na makampuni kote duniani.
Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa leo na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), ‘Downdetector’ ambayo hufuatilia kukatika kwa huduma hiyo, iliripoti matatizo milioni 10.6 ya kukatika kwa huduma hiyo kote duniani, ikiwa ni idadi kubwa zaidi kuwahi kurekodiwa.
Pia kukatika kwa huduma hiyo kumepelekea utajiri wa Mark Zuckerberg kushuka kwa zaidi ya dola za Marekani bilioni sita, na kumfanya kushuka hadi nafasi ya tano, na kuwa nyuma ya Bill Gates, katika orodha ya matajiri duniani.
Aidha, taarifa imeeleza kuwa, kwa wengi kupotea kwa huduma hiyo ulikuwa usumbufu mkubwa, wakiwemo wafanyabiashara, ambapo wengine waliokosa njia nyingine za kuaminika kuwasiliana na wateja wao.
Imeripotiwa kuwa maeneo ya kazi yakiwemo mashirika, taasisi na makampuni ambayo wafanyikazi wake wamekuwa wakifanyia kazi nyumbani au mashambani kutokana na mlipuko wa Uviko-19, yaliathirika sana kutokana na kutegemea WhatsApp kwa ajili ya kuwasiliana.