KAMPUNI ya uuzaji wa samani za nyumbani na ofisini pamoja na mavazi ya GSM, imezindua mashindano mawili ya ‘Shinda na ung’arishe nyumba yako’ pamoja na ‘Jishindie Safari ya Utalii Ngorongoro’ kutoa nafasi kwa wateja kujishindia zawadi wakati wa msimu huu wa sikukuu.
Mashindano hayo yatahusisha maduka yote ya Dar es Salaam ambayo ni Mlimani City, Msasani Mall, GSM Pugu Mall, GSM Home Mikocheni, Aura Mall na yale ya mikoa ya Dodoma na Arusha.
Wataaoshiriki katika mashindano hayo watajishindia samani na nguo katika msimu wa sikukuu za mwisho wa mwaka.
Akizungumza Dar es Salaam jana, baada ya kuzindua mashindano hayo Mlimani City, Ofisa biashara wa GSM, Allan Chonjo alisema lengo la kuanzisha shindano hilo ni kuwafurahisha wadau wake.
“Mwaka 2020 umekuwa na changamoto nyingi hususan mlipuko wa corona ambao umeathiri shughuli za kijamii na kuharibu mipango na malengo ambayo watu walikuwa wamejiwekea.
“Kwa kulitambua hili GSM tukaona hatuna budi kuanzisha shindano hili ili kila mmoja aweze kupata nafasi ya kujishindia bidhaa aliyokuwa akiitamani kuimiliki kutoka GSM Home na GSM Retail,” alisema Chonjo.
Alisema shindano hilo lilianza rasmi Desemba Mosi na linatarajiwa kufanyika kwa awamu nne, kila awamu mshindi atapatiwa zawadi maalumu kutoka GSM Home au GSM Retail.
“Kila mtu ana fursa ya kushiriki kwa kujipatia kuponi baada ya kununua bidhaa yoyote yenye thamani ya kuanzia Sh milioni moja na kuendelea kuingia kwenye droo,”
Kwa upande wa mavazi alisema mteja akinunua nguo zenye thamani ya zaidi ya Sh 50,000 kwa mara moja ataingia kwenye droo na kujipatia zawadi mbalimbali ikiwemo zawadi ya kulipiwa safari ya kwenda kutalii Ngorongoro kwa watu wawili.