Licha ya biashara mbalimbali kupita katika msukosuko wa kiuchumi, faida baada ya kodi katika benki zinazotoa huduma nchini imeongezeka kwa takriban mara saba zaidi kutoka Sh133.89 bilioni mwaka 2018 hadi Sh934.38 bilioni mwaka 2022.
Katika miaka ya karibuni uchumi wa dunia umekumbwa na athari kubwa zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, majanga ya Uviko-19 na vita vya Russia na Ukraine, hali iliyosababisha ukuaji wake kutokuwa wa kasi inayotabirika.
Hata hivyo, Licha ya mambo hayo kuibua changamoto za kiuchumi katika nyanja mbalimbali, sekta ya benki imeshuhudia ukuaji mkubwa katika viashiria vyote vya ukuaji, huku faida ikiongezeka maradufu, ikilinganishwa na miaka mitano iliyopita.
Kupitia ripoti tofauti za BoT, Mwananchi limefanya uchambuzi wa vipengele tofauti vya ufanisi wa benki katika kipindi hiki, ikilinganishwa na miaka mitano iliyopita na kuangazia sababu za kuongezeka kwa faida za wakopeshaji hao katika nyakati ngumu za kiuchumi.