Tume ya ushindani Tanzania (FCC) imesema kwa mwaka 2022/23 imefanya mapambano dhidi ya bidhaa bandia ambapo katika kaguzi zake kwenye Bandari ya Dar es Salaam na Bandari Kavu (ICDs) asilimia 3.4% ya jumla ya makasha (containers) yaliyokaguliwa yenye thamani ya kiasi cha Tsh bilioni 20.8 yalikutwa na bidhaa zilizokiuka sheria ya alama za bidhaa
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Tume hiyo Willam Erio wakati akieleza utekelezaji wa majukumu ya Tume hiyo na mwelekeo wa utekelezaji wa mwaka wa fedha 2023/24 katika mkutano na Waandishi wa Habari leo, Jumatano Agosti 2.2023 katika ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Jijini Dodoma
Ameendelea kufafanunua kuwa kaguzi za kushtukiza (Dawn Raids) nazo zilifanyika ambapo bidhaa zenye thamani ya shilingi Billioni 4.7 zilizokiuka sheria ya alama za bidhaa zilikamatwa na hatua stahiki zilichukuliwa na kuongeza kuwa kaguzi hizo zilifanyika katika mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi, Ruvuma, Songwe, Kilimanjaro, Pwani, Mwanza, Arusha, Katavi na Mbeya
“FCC imefanya uharibifu wa bidhaa bandia zilizokamatwa katika Mikoa ya Mbeya, Iringa na Ruvuma. Bidhaa zilizoharibiwa ni pamoja na wino wa printa katoni 432 na kilo 1,302 za vifungashio"
Mbali na hayo tume hiyo imepokea malalamiko 58 ya watumiaji wa bidhaa na huduma yanayohusu mikataba inayoandaliwa na upande mmoja (1), usalama wa bidhaa, upotoshaji katika bidhaa, huduma za kifedha na huduma za Bima
Pia Malalamiko 21 yaliyohusu masharti ya mikataba inayoandaliwa upande mmoja (1) yalipatiwa ufumbuz, pia Malalamiko yaliyohusu upotoshaji wa bidhaa yalipatiwa ufumbuzi na Malalamiko 13 yaliyohusu huduma za fedha, usalama wa bidhaa na huduma na bima ambayo yalihamishiwa katika Mamlaka sahihi ambazo ni TBS, BOT na Jeshi la Polisi
“Malalamiko 19 yako katika hatua mbalimbali za kupatiwa ufumbuzi, FCC imesajili mikataba 77 iliyoandaliwa na upande mmoja (Standard Form Consumer Contracts) kutoka katika sekta mbalimbali lengo la kusajili mikataba hiyo ni pamoja na kuondoa masharti kandamizi, urahisi wa kueleweka kwa mikataba kwa kutumia lugha rahisi na kuhakikisha mikataba hiyo inazingatia misingi ya ulinzi wa mlaji."