Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Exim yasaini makubaliano na kampuni za Indesso kukuza kilimo

Exim Yasaini Makubaliano Na Kampuni Za Indesso Kukuza Kilimo Exim yasaini makubaliano na kampuni za Indesso kukuza kilimo

Thu, 24 Aug 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Benki ya Exim imesaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na kampuni za Indesso na Amani Essence ili kushirikiana katika kukuza maendeleo ya sekta ya kilimo nchini Tanzania.

Mkataba huo uliosainiwa wakati Kongamano la Biashara la Indonesia na Tanzania lililofanyika jijini Dar es Salaam juzi unaunga mkono utetekeleza Ajenda ya 10/30 ya Wizara ya Kilimo inayolenga kufikia kiwango cha ukuaji cha asilimia 10 kwa sekta hiyo ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza mara baada ya utiaji saini huo, Mkuu wa Kitengo cha Wateja Wadogo wa Benki ya Exim Andrew Lyimo alisema hatua hiyo ni kubwa na inalenga kuongeza thamani ya sekta ya kilimo kwa kuwawezesha wafanyabiashara wa karafuu kupata mikopo kwa urahisi.

"Kwa mujibu wa makubaliano yetu, Benki ya Exim itakuwa mfadhili wa mitaji kwa Biashara Ndogo na za Kati (SMEs) zinazojishughulisha na usindikaji wa majani ya karafuu ili kukamua na kusafisha mafuta ambaye badaye yatasafirishwa kwenda nchini Indonesia," alisema Lyimo.

Lyimo alisema benki yake imejipanga kuendelea kuchangia maendeleo ya sekta ya kilimo biashara kote nchini na kuongeza kuwa itatoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa mitambo ya kukamua mafuta hayo muhimu kutoka kwenye majani ya mikarafuu.

Alisema hapo awali, majani ya mikarafuu yaliyoanguka hayakuwa na matumizi na yalichukuliwa kama takataka na kuongeza kuwa kutokana na makubaliano hayo mapya, wakulima wanaojishughulisha na uzalishaji wa zao la karafuu wanaweza kubadilisha majani hayo kuwa fedha.

"Wakulima wa karafuu sasa wataweza kutoa majani na kuyauza kwa watu wenye mashine za kutengeneza mafuta ya kula," alisema.

Lyimo katika hafla hiyo alisisitiza dhamira ya benki hiyo kuendelea kuwekeza katika kuendeleza kilimo biashara na sekta ya kilimo kwa ujumla.

"Tutaanza kutekeleza ushirikiano huu mpya katika mikoa ya Tanga na Morogoro ikiwa ni utekelezaji wa dhamira yetu kuendelea kuunga mkono juhudi zinazoendelea kufanywa na Serikali ya awamu ya sita kukuza maendeleo ya sekta ya kilimo kwa uwezo wetu wote," alisisitiza.

Alisisitiza tena kuwa benki yake itaendelea kufanya kazi kwa karibu na wadau mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa sekta ya kilimo ili kuchangia maendeleo ya sekta hiyo nchini Tanzania kupitia utoaji wa mikopo na uwekezaji.

“Kama benki, tutaendela kujitolea kwa kubuni mbinu mpya za ufadhili ili kuwapatia wafanyabiashara wadogo na wa kati wanaoshughulika na usindikaji wa mafuta kutoka kwenye karafuu kupata suluhu maalum za kifedha na kuhakikisha wanaongeza uzalishaji. Tunaamini juhudi zetu zitasaidia pakubwa katika kuongeza uzalishaji wao na vipato vyao kwa jumla,” aliongeza.

Naye Mkurugenzi wa Indesso Feri Agustain wakati wa hafla hiyo alisema “Indesso inafuraha kuimarisha ushirikiano wetu na Benki ya Exim na tunaamini ushirikiano huu utasaidia kukuza sekta ya kilimo endelevu nchini Tanzania.

Agustain alisema kuongeza ushirikiano na Benki ya Exim ni muhimu katika kuendeleza masuluhisho ya kibunifu ya kifedha ambayo yatawawezesha wakulima wa karafuu kupata fedha.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live