Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Exim Bank, Wakala wa Serikali Zanzibar wasaini mkataba wa makubaliano

Exim Bank, Wakala Wa Serikali Zanzibar Wasaini Mkataba Wa Makubaliano Exim Bank, Wakala wa Serikali Zanzibar wasaini mkataba wa makubaliano

Sun, 10 Sep 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Benki ya Exim Tanzania imesaini Mkataba wa Makubaliano (MoU) na Wakala wa Serikali Mtandao Zanzibar (eGaz) unaolenga kuchochea safari ya mageuzi ya kidijitali Zanzibar.

Makubaliano hayo yametiwa saini baada ya uzinduzi wa hivi karibuni wa Mkakati wa Serikali ya Kidijitali Zanzibar wa mwaka 2023-2027 uliozinduliwa na Dk Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.

Akizungumza kabla ya utiaji saini huo uliofanyika visiwani Zanzibar mwishoni mwa wiki, Afisa Mkuu wa Fedha wa Benki ya Exim (CFO) Shani Kinswaga alisema utiaji saini wa Mkataba huo mpya unaendana na malengo ya mageuzi ya kidijitali ya Zanzibar yaliyoainishwa katika Mpango wa Uchumi wa Kidijitali wa Kisiwa hicho.

Kinswaga alisema benki hiyo itatumia teknolojia kama dhana ya kutoa huduma za kipekee za kidijitali kwa kushirikiana na eGaz kufanya malipo ya kidigitali ambayo hatimaye yataongeza mapato ya Serikali ya Zanzibar na kuboresha ufanisi.

“Ushirikiano huu mpya unasisitiza dhamira ya benki ya Exim ya kuchangia maendeleo endelevu ya kiuchumi visiwani Zanzibar. Kama benki, tunaamini kwamba makubaliano yaliyofikiwa leo sio tu yatachangia pakubwa katika ukuaji wa uchumi imara lakini pia yatasaidia kuharakisha mabadiliko ya Zanzibar katika uchumi imara wa kidijitali,” Kinswaga alisema.

Kinswaga alibainisha kuwa mwanzoni mwa mwaka huu, benki ya Exim iliboresha mfumo wake na kuweka miundombinu thabiti, hatua inayolenga kuimarisha utendaji wake na kuwapa wateja hali ya juu ya usalama, ufanisi na uvumbuzi.

"Kama benki, tutaendelea kuwekeza katika teknolojia ili kuongeza uwezo wa mifumo yetuna kutoa huduma bora kwa wateja wetu , jamii inayotuzunguka na taasisi mbalimbali za Serikali visiwani hapa," Kinswaga alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Serikali Mtandao Zanzibar (eGaz) Said Seif Said alibainisha kuwa ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ni wa kimkakati na utasaidia kukuza uchumi na kuwezesha ushirikishwaji wa kifedha na kidijitali visiwani Zanzibar.

“Huu ni ushirikiano wa aina yake na umekuja kwa wakati muafaka. Tumekuwa tukingojea wakati huu kwa muda mrefu na tunafurahi kwamba hatimaye tumetia saini makubaliano leo kuashiria mwanzo wa safari yetu ya mabadiliko ya kidijitali,” alisema Said.

Said alibainisha kuwa taasisi yake itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Benki ya Exim ili kutekeleza mpango wa Uchumi wa Kidijitali wa Zanzibar.

“Tunapoanza safari hii ndefu ya kutekeleza Mkakati wa Serikali ya Dijitali ya Zanzibar wa miaka mitano, tunafurahi kwamba wadau wetu wa kimkakati kama Benki ya Exim wamejitokeza kutuunga mkono na tunaamini mkakati huo sasa utafikiwa katika kipindi kifupi zaidi ili kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali,” alisema.

Said aliongeza kuwa mabadiliko ya kidijitali ni kipaumbele cha kimkakati kwa Serikali ya Zanzibar na kuongeza kuwa taasisi yake imejipanga kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma za kidigitali kwa kutumia zana mbalimbali za kidijitali zikiwemo simu za kisasa.

"Ushirikiano huu utatuwezesha kuendesha shughuli zetu kwa ubunifu kwa kutumia teknolojia ya kisasa ya Benki ya Exim ili kutoa huduma za kidijitali hapa visiwani Zanzibar," aliongeza.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live