Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) imezindua mpango mkakati wa kuongeza maradufu mauzo ya matunda na mbogamboga nje ya ukanda huo hadi kufikia Dola milioni 900 katika miaka nane ijayo.
Katika mpango Mkakati wa Mwaka 2021-2031 uliozinduliwa mwishoni mwa mwaka jana, EAC inapanga kuongeza eneo la uzalishaji wa matunda kwa asilimia tano hadi hekta milioni 10 ili kushika soko la kimataifa la mauzo ya nje.
Ikiwa utatekelezwa, biashara ya ndani ya EAC ya bidhaa za matunda na mboga itaongezeka kutoka Dola milioni 9.9 za sasa hadi Dola milioni 25 ifikapo mwaka 2031.
Ukanda huo pia unatarajia kuongeza eneo la uzalishaji wa mbogamboga kwa asilimia tano hadi hekta milioni 45 kutoka hekta milioni 32.8, huku uzalishaji ukiongezeka kwa angalau asilimia tatu.
"Ukiangalia Mpango Mkakati wa Mwaka 2021 hadi 2031, EAC inazalisha aina mbalimbali za matunda na mbogamboga zinazoweza kusafirishwa kwenye masoko ya kikanda na kimataifa," alisema Naibu Katibu Mkuu wa EAC, anayeshughulikia masuala ya uzalishaji na kijamii, Christopher Bazivamo.