Dar es Salaam. Serikali imesema Sh302. 63 bilioni zimekusanywa katika sekta ya madini kuanzia Julai Mosi, 2018 hadi sasa, kiasi ambacho hakijawahi kukusanywa katika sekta hiyo.
Hayo yameelezwa leo Alhamisi Mei 30, 2019 na msemaji wa Serikali, Dk Hassan Abbas katika mkutano wake na waandishi wa habari, akibainisha kuwa mafanikio hayo yametokana na mageuzi yaliyofanywa na Serikali iliyopo madarakani.
Amesema mabadiliko hayo yameipa heshima Tanzania na kuifanya kuwa mfano kwa nchi ya Afrika katika kuwabana wanyonyaji walioweka mizizi kwenye sekta hiyo.
“Watafiti wengi wanafanya tafiti kujua ni namna gani Tanzania imefikia hatua hiyo. Kuna nchi nyingi zimeanza kufuata nyayo zetu kwa kifupi tumejiwekea heshima kubwa,” amesema Dk Abbas.
Amesema siri kubwa ya mafanikio hayo ni kuongeza usimamizi, ufuatiliaji na kuwekwa mifumo ya kisayansi.
Licha ya kuanzishwa ndani ya muda mfupi masoko ya madini katika mikoa mbalimbali nchini yametajwa kuwa na mchango mkubwa katika sekta hiyo na kuzuia mianya ya utoroshaji wa madini vitendo vilivyokuwa vinaminya mapato ya Serikali.
Pia Soma
- Mashahidi wakwamisha kesi ya 'Mpemba wa Magufuli'
- UDSM, China kushirikiana kufanya tafiti
- Mwenyekiti UVCCM ataja sababu wagombea CCM kutokubalika