MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), imesema kampuni ya DP World ya Dubai katika Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) imeanza kushusha vifaa katika Bandari ya Dar es Salaam kuanza uwekezaji.
Aidha, TPA imebainisha kuwa makabidhiano ni tangu Aprili 7, mwaka huu bila kuathiri uendeshaji wa bandari hiyo. Mkurugenzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Mrisho Mrisho alisema hayo Dodoma akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Plasduce Mbossa katika Mkutano wa 13 wa Mwaka wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF).
Mrisho alisema DP World ambao wataendesha gati namba moja hadi saba, wameshusha meli nzima yenye vifaa vya kisasa ikiwamo mashine nane za RTG, mashine nyingine 19 za kushusha kontena, jenereta kubwa za kuendesha mashine hizo na mashine nyingine nne ziko njiani.