Mirerani. Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, mhandisi Zephania Chaula amevunja mkutano wa wamiliki wa migodi na wanunuzi wa madini ya Tanzanite.
Walikutana katika mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa Luka katika mji mdogo wa Mirerani kujadili namna ya kuingia katika eneo la mgodi wa madini ya Tanzanite lililozungushiwa ukuta.
Kufatia uamuzi huo wachimbaji hao waliokuwa wakiongozwa na mwenyekiti wa chama cha wachimbaji madini wa Mkoa wa Manyara (Marema), Sadiki Mneney na mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Simanjiro, Awadhi Omary walilazimika kuondoka eneo hilo.
Wakati Mneney akifungua mkutano huo mkuu wa kituo cha polisi Mirerani, Evarest Makala alifika na kuagiza kikao hicho kivunjwe, kueleza kuwa ni agizo kutoka kwa mkuu wa wilaya hiyo.
Akizungumza na MCL Digital leo Alhamisi Julai 19, 2018, Mneney amesema lengo la kikao hicho ilikuwa kujadili changamoto wanazozipata wakati wa kutoka na kuingia katika mgodi huo, kwa maelezo kuwa hata magari yamezuiwa kutoka wala kuingia.
Soma Zaidi:
Kuingia Mirerani sasa kwa vitambulisho vya Taifa
“Ukitaka kuingia inapaswa uwe na kitambulisho cha Taifa na kile cha Wizara ya Madini na wengi wao hawana. Sasa magari yaliyobeba maji hayaingii wala kutoka ndani na hivyo kukwamisha shughuli zetu,” amesema.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti amesema wamiliki wa migodi na wachimbaji wa madini wanapaswa kutii maagizo ya Serikali ya namna ya kuingia na kutoka ndani ya ukuta huo unaozunguka migodi ya Tanzanite.