Dar es Salaam. Serikali ya China imesema haitaliacha Shirika la Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) life bali itaendelea kufanya kazi na nchi hizo mbili ili kuhakikisha usafiri huo ulioanza miaka 40 iliyopita unadumu.
Akizungumza katika ofisi za kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) Tabata Relini jijini Dar es Salaam, Balozi wa China nchini Tanzania, Wang Ke amesema Tazara ni umoja wa nchi za Tanzania, Zambia na China na inapaswa kuendelea kuwapo.
Amesema ujenzi wa reli hiyo kati ya Dar es Salaam na Kapiri Mposhi uliofanyika kati ya mwaka 1970 hadi 1976 ilikuwa ni zawadi ya China kwa mataifa ya Zambia na Tanzania, hivyo nchi hizo zinapaswa kuendelea kushirikiana.
Akizungumzia taarifa za vyombo vya habari kuwa Tanzania ilitaka kuboresha masharti matano yaliyohusu mradi wa Bandari ya Bagamoyo kwa sababu hayakuwa na faida kwa Serikali ya Tanzania, amesema taarifa hizo hazina ukweli wowote.
Ke amesema taarifa hizo zimeandikwa mtandaoni kutoka Kenya na si kwenye gazeti na wenyewe kama ubalozi hawafahamu zilitoka wapi.
Alisema mradi huo wa Bandari ni muhimu na unahusu Serikali na mwekezaji kutoka China ambao ndiyo wanaopaswa kuzungumzia ni namna gani wanaweza kuuendeleza.
Pia Soma
- Shahidi aeleza alivyopata taarifa za mkutano wa Zitto
- Maombi ya wadau kwa Serikali ya Tanzania kuhusu ubunifu haya hapa
- Lukuvi apiga marufuku maofisa ardhi kutoa ofa za viwanja