Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

China yaunda meli ya kubeba makontena 24,116

China China Meli China yaunda meli ya kubeba makontena 24,116

Fri, 10 Mar 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

China imeweka rekodi mpya duniani kwa kuunda meli kubwa yenye uwezo wa kubeba makontena 24,116 pamoja na mizigo ya tani zaidi ya 240,000.

Taarifa iliyochapishwa kwenye Tovuti ya Gazeti la Umma la nchini humo leo Machi 10, 2023 kupitia mtandao wa ‘swahili people’, imeeleza kwamba kukamilika uundaji wa meli hiyo huko Shanghai, China, ni rekodi mpya ukilinganisha na meli iliyoundwa mwaka jana yenye uwezo wa kubeba makontena 24,000.

Kampuni tanzu ya Shirika la Uundaji Meli la China imesema tayari kazi ya uundaji imekamilika kwenye kituo cha uundaji wa meli cha Changxing cha Shirika la Uundaji Meli la China.

“Hii ni meli kubwa zaidi iliyoundwa na kukamilika duniani, ambayo imevunja rekodi ya “Meli ya Changyi” iliyokamilika Mwezi Juni, Mwaka 2022 yenye uwezo wa kubeba makontena 24,000,” imenukuliwa sehemu ya taarifa hiyo.

Meli hiyo imesanifiwa kwa kujitegemea na Kampuni ya Hudong Zhonghua. Ina urefu wa jumla wa mita 399.99, upana wake ni mita 61.5 na kimo chake ni mita 33.2.

Pia inaweza kubeba makontena kwenye ngazi 25, ambazo ni sawa na urefu wa jengo lenye ghorofa 22 na inaweza kubeba mizigo ya tani zaidi ya 240,000.

Meli hiyo inaweza kubeba makontena 24,116 yenye kipimo cha kawaida na inatajwa kuwa meli yenye uwezo wa kubeba makontena mengi zaidi kwenye bahari kuliko meli nyingine zote kwa hivi sasa.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live