Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyabiashara wenye Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA ) Wilaya ya Rufiji na Kibiti Mkoa wa Pwani, Maxmillian Masero amesema wakulima nchini Tanzania wanakabiliwa na changamoto kuu mbili za uzalishaji na uhifadhi.
Ametoa kauli hiyo leo jioni Mei 23, 2019 katika mjadala wa Jukwaa la Fikra kuhusu kilimo lililoandaliwa na kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL) linalofanyika katika ukumbi wa Kisenga na kurushwa moja kwa moja na kituo cha Televisheni cha ITV na Reduio One.
Masero amesema mara nyingi mazao yanaharibika shambani kwa kushambuliwa na wadudu, wakati mwingine huoza kwa kukosa huduma bora.
Ameishauri Serikali kutoa elimu kwa wakulima jinsi ya kuhudumia mazao kwa ajili ya kuepuka changamoto hizo ambazo zinachochea uvunaji hafifu.
“Changamoto nyingine ni uhifadhi ambapo mkulima baada ya kuvuna mazao yanaharibikia nyumbani kwa kukosa uhifadhi bora kwa ajili ya matumizi ya baadaye,” amesema Masero.
Amesema ili kudhibiti uharibifu wa mazao baada ya kuvuna inatakiwa kujenga maghala ya kutosha kwa ajili ya kuhifadhi mazao ya wananchi.
Pia Soma
- Ansaf yataja suluhisho la changamoto tano za Kilimo
- Mtafiti wa kilimo ayataja maeneo matatu yanayoweza kufanikikisha sekta ya kilimo Tanzania
- Licha ya changamoto kilimo, bado kinasonga mbele – Profesa Nyange
“Unakuta mkulima anavuma halafu anaambiwa asiuze mazao yake hadi asubiri uamuzi kutoka juu na wakati huo unakuta mwananchi hajui jinsi ya kuhifadhi,” amesema.
Pia, alizungumzia miundombinu ya usafirishaji akibainisha kuwa si rafiki kwa wakulima hasa wanaosafirisha mazao yao kutoka kijijini kuja mjini.
“Tunafahamu kilimo kina mchango mkubwa katika taifa letu lakini hatuwezi kufika mbali kama hatutatoa kipaumbele kwa wakulima ambao ndiyo wazalishaji wakubwa wa malighafi ambazo tunategemea kutumika katika viwanda vyetu,” amesema.