Mtwara. Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela) imewataka wafanyabiashara kutumia njia ya mtandao kusajili na kupata utambulisho wa bidhaa wakiwa ndani na nje ya Tanzania.
Akizungumza leo Alhamisi Juni 27, 2019 katika mafunzo ya kuwajengea uelewa wafanyabiashara mkoani Mtwara, mkurugenzi wa utawala na fedha kutoka Brela, Bakari Mketo amesema kundi kubwa la wafanyabiashara mkoani humo hawana elimu ya usajili wa biashara zao.
Amesema hatua hiyo inasababisha baadhi ya bidhaa zao kutotambulika na kukosa masoko ya uhakika.
“Baadhi ya wafanyabiashara wanakosa fursa ya masoko ndani na nje ya nchi kutokana na bidhaa zao kutotambulika, watu wengi wanaponunua bidhaa huwa wanapenda kujua ni ya nani na inatoka wapi na pale anapokutana na bidhaa ambayo haitambuliki inakuwa inampa wasiwasi,” amesema Mketo
Mwakilishi kutoka Wizara ya Viwanda na Biashara, Lilian Godwin amesema wakati Serikali na wadau wakitekeleza adhima ya viwanda wafanyabiashara wakubwa na wadogo wanaguswa kwa lengo la kukuza uchumi na wamekua wakisimamia viwanda vidogo na vikubwa kuona ubora unaotakiwa na uzalishaji weye tija.
Mmoja wa wafanyabiashara, Mwajuma Ankoni amesema, “Tumekuwa tukifanya bila kujua umuhimu wa kujisajili Brela kutokana na kutokufahamu.”
Pia Soma
- Zitto ataka Bunge kuibana Serikali ya Tanzania kuhusu kukopa
- Tiba asili za barabarani zapigwa marufuku Iringa
- Nyama ya nyumbu yampandisha kortini mtumishi wa hifadhi ya Ikona
- Kiongozi wa mbio za Mwenge amgomea Mkuu wa Wilaya ya Mwanga