Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

BoT yaagiza Vicoba, Saccos kuwasilisha taarifa wiki ijayo

Sat, 5 Jan 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Ephrahim Bahemu, Mwananchi [email protected]

Dar es Salaam. Waendeshaji wote wa taasisi ndogo za fedha nchini vikiwamo Vicoba na Saccos, sasa watakuwa wakifanya shughuli zao chini ya usimamizi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na kuanzia wiki ijayo, watatakiwa kuwasilisha baadhi ya nyaraka.

Novemba 16, mwaka jana, Bunge lilipitisha Sheria ya Usimamizi wa Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2018 kwa lengo la kusaidia utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya 2017.

Desemba 31, mwaka jana, BoT ilitoa taarifa kwa umma ikiwataka watu wote wanaofanya biashara ya huduma ndogo za kifedha kuwasilisha taarifa zao za uendeshaji na wasimamizi wa taasisi hizo kwa chombo hicho cha juu katika usimamizi wa sekta ya fedha kabla ya Januari 11.

“Watu wote wanaofanya biashara hiyo katika sekta ndogo ya fedha wanapaswa kuwasilisha cheti cha kutambuliwa kama wamiliki, leseni ya biashara iliyotolewa na Wakala wa Usajili wa Biashara (Brela), leseni na anuani ya mahali biashara ilipo na mawasiliano,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.

Pia, iliyataja mambo mengine yanayopaswa kuwasilishwa kuwa ni ya aina ya huduma zinazotolewa na taarifa endapo kuna ukaguzi wa hesabu unaofanyika kila mwaka sambamba na orodha ya wamiliki wa biashara, bodi ya wakurugenzi, mtendaji mkuu wa taasisi na uraia wao.

Kadhalika, taarifa kuhusu mfumo unaotumika katika uhifadhi wa fedha na teknolojia ya mawasiliano pamoja na taarifa za vitega uchumi, madeni na thamani ya hisa za kila mmiliki.

Aidha, katika sheria hiyo mpya katika kifungu chake cha 12 pamoja na mambo mengine, imeipa mamlaka BoT kutoa leseni, kusimamia na kudhibiti sekta ya taasisi ndogo za fedha na kifungu cha 16 kimezuia mtu ambaye hana leseni kujihusisha na biashara hiyo.

Katika sheria hiyo biashara ya taasisi ndogo ya fedha imetafsiriwa kama biashara inayohusisha kupokea fedha kama amana au akiba, kutoa mikopo na ukopeshaji kwa wajasiriamali wadogo na watu wa kipato cha chini.



Chanzo: mwananchi.co.tz