Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Biteko auonya  uongozi Stamigold

5eab40debf7ea7c800cbbe94c371617c.jpeg Biteko auonya  uongozi Stamigold

Thu, 15 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAZIRI wa Madini, Doto Biteko ameuagiza uongozi wa mgodi wa Stamigold akiwemo Meneja Mkuu, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji, Bodi, menejimenti na wafanyakazi wajitafakari kama utendaji wao una manufaa kwa taifa.

Biteko alitoa agizo hilo Biharamulo, mkoani Kagera alipotembelea mgodi huo ambao ni kampuni tanzu ya Shirika la Madini la Taifa (Stamico).

Aliieleza menejimenti na wafanyakazi wa mgodi huo kuwa, serikali inachukizwa na vitendo vya utoroshaji dhahabu vinavyofanywa na baadhi ya watumishi.

"Mungu amewapa bahati ya kuwa kwenye mgodi huu, nawasihi sana uleeni, mkiulea na nyinyi utawalea. Shirika hili likifa wengi mtapoteza ajira na kukosa mishahara" alisema Biteko.

Alimuagiza Mwenyekiti wa Bodi ya Stamico kuwachukulia hatua za kiutumishi watuhumiwa waliopo mahakamani kwa kuzingatia taratibu wa utumishi.

Meneja Mkuu wa mgodi huo, Gilay Shamika alisema wafanyakazi wanafanya kazi kwa kujituma na kulinda madini katika mgodi huo.

Aliipongeza Stamico kwa kuendekea kufanikisha shughuli za uwekezaji katika mgodi huo.

Katika ziara hiyo, Biteko alijionea miundombinu ya mgodi huo ukiwamo mtambo wa uchenjuaji dhahabu na bwawa la kuhifadhia topesumu.

Waziri huyo pia alitembelea mgodi wa wachimbaji wadogo wa dhahabu Matwiga na kuzungumza na wachimbaji kuhusu changamoto zinazowakabili.

Viongozi wengine waliokuwa kwenye ziara hiyo ni Mkuu wa Wilaya ya Biharamulo, Kimelembe Rwota, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Stamico, Dk Venance Mwasse, Ofisa Madini Mkazi Mkoa wa Geita, Lucas Mlekwa, Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Ramadhani Lwamo, na Kaimu Kamishna wa Madini, Zephania Nsungi.

Chanzo: www.habarileo.co.tz