Naibu Waziri Mkuu, Dk Doto Biteko ameitaka Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (Tafiri), isione fahari kuona wavuvi wanaendelea kuwa masikini.
Ametaka fahari ya taasisi hiyo, itokane na kuwaona wavuvi wanakuwa na maisha bora yatakayojengwa na shughuli zao.
Dk Biteko ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam leo Alhamisi Oktoba 26, 2023 alipohutubia sherehe za kufunga maadhimisho ya miaka 40 ya Tafiri.
Katika hotuba yake hiyo, ametaka utendaji wa taasisi hiyo uwafanye wavuvi waione ndiyo kimbilio lao.
"Waziri (Mifugo na Uvuvi- Abdallah Ulega) bado una kazi ya kufanya wewe na watu wako (Tafiri), mnapaswa kuhakikisha mnakuwa kimbilio la wavuvi, oneni fahari kuwaona wavuvi wanakuwa matajiri na sio masikini," amesema.
Naibu Waziri Mkuu huyo, amesema wakati Tafiri inasherehekea miaka 40 ya kuanzishwa kwake, ni vyema ijikite katika mtazamo wa iliyoyafanya kuwaunufaisha wavuvi.
Kuhusu biashara ya samaki, amesema mwaka jana mauzo yalikuwa Dola za Marekani 168 milioni na mwaka huu hadi sasa yamefikia Dola za Marekani 249 milioni.