Mkuu wa Mkoa wa Geita, Martin Shigella amesema Serikali imeanza ujenzi wa mradi mkubwa wa maji wenye thamani ya shilingi bilioni 130 kutoka Ziwa Victoria kwenda katika mkoa wa huo ili kumaliza tatizo la maji.
Akitoa salamu za mkoa huo kwenye Misa Takatifu ya Sikukuu ya Krisimasi kitaifa inayofanyika mkoani Geita, Shigella amesema utekelezaji wa mradi huo umeanza na kutakuwa na matanki makubwa yatakayohudumia maji kwenye mkoa huo.
Amesema kuwa mbali na mradi wa maji Serikali pia imetoa pesa kwa ajili ya ujenzi wa stendi mpya na ya kisasa ambayo itakuwa stendi ya mabasi ya mkoa huo.
Ameongeza kuwa, upembuzi yakinifu wa ujenzi wa barabara inayounganisha mkoa huo na mkoa wa Shinyanga umekamilika na kibali cha fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kimeombwa ili ijengwe na kuunganisha mkoa huo na mikoa mingine.