Akizungumzia DCPC, Chalamila alisema mkoa unawategemea katika kufanya maendeleo ikiwamo kumpa ushauri wa nini wangependa kuona kinafanyika ili mkoa uwe wa kuvutia machoni mwa watu na kuutofautisha na mingine. Chalamila alikubali kuwa mlezi wa klabu hiyo baada ya kuombwa na DCPC.
Apewa tuzo ya Rais Samia
Katika hatua nyingine, Chalamila alipokea tuzo kwa niaba ya Rais Samia Suluhu Hassan, iliyotolewa na DCPC ikiwa ni kutambua mchango wake katika kuboresha tasnia ya habari.
Akieleza sababu ya kumpa Rais Samia tuzo hiyo, Katibu wa DCPC, Fatma Jalala alisema chini ya utawala wake amefanya maboresho mbalimbali ikiwemo kuiunganisha Wizara ya Habari na Wizara ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano ili kuleta tija na ufanisi.
"Ametimiza ahadi ya kurekebisha sheria ya huduma za vyombo vya habari ya mwaka 2016 na tunaamini utaendelea kuiboresha ili kukidhi mahitaji ya wadau na kuweka mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji," alisema Fatma.
Akimkaribisha Chalamila, Makamu Mwenyekiti wa DCPC, Salome Gregory, aliahidi klabu hiyo kuendelea kumpa ushirikiano pamoja na ofisi yake ili kufikia malengo ya maendeleo yaliyowekwa na mkoa na Taifa kwa ujumla