Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Benki zaingia makubaliano kukopesha wajasiriamali bila riba

FEDHA WEB Equity, ZEEA na SMIDA zaingia makubaliano kukopesha wajasiriamali bila riba

Fri, 24 Mar 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Benki ya Equity Tanzania imeingia makubaliano ya kufanya kazi na Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (ZEEA) na Wakala wa Maendelo ya Viwanda Vidogo na vya kati visiwani Zanzibar (SMIDA) kwa lengo la kutoa mikopo nafuu bila riba kwa wajasiriamali wakubwa na wadogo.

Kuingia makubaliano hayo na ZEEA na SMIDA ni sehemu ya mkakati wa benki hiyo kukuza uchumi na kuinua kipato cha wateja wake.

Hafla hiyo imehudhuriwa ma Waziri wa Nchi ofisi ya Rais-Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mudrick Soraga.

Mkurugenzi Mtendaji wa Equity, Isabela Maganga alimuhakikishia Waziri kwamba benki hiyo itaunga mkono juhudi kubwa zinazofanywa na marais Dr Hussein Mwinyi na Samia Suluhu Hassan.

Katika makubaliano hayo yaliyoingiwa na pande zote tatu, benki hiyo inakwenda kutoa mikopo bila riba kwa wananchi wa Zanzibar

“Makubaliano haya yanakwenda kuleta mageuzi makubwa sana katika sekta ya fedha na uchumi kwani yatawezesha taasisi zetu kuleta maendeleo ya haraka kwa vijana, si tu maendeleo bali kukuza elimu ya fedha na ukopaji wenye malengo na tija.Makubaliano haya yatasaidia katika suala zima la kuongeza ajira kupitia nguzo ya ujasiliamali kwani wajasiliamali watapata mitaji ya kutosha kukuza biashara zao sambamba na kuongeza ubunifu,” amesema Mkurugenzi wa Equity.

Taarifa ya benki ya Equity imesema mambo mengine mahususi ni pamoja na kutumia uzoefu wa ufuatiliaji mikopo ili kuhakikisha kuwa pesa inayokopeshwa pasi na riba inarejeshwa kwa wakati na kulingana na vigezo na masharti yaliyokubaliwa, kutoa taarifa kwa vyombo wabia (ZEEA na SMIDA) juu ya ufanisi wa programu hiyo kwa wakati na kutoa mikopo kwa wakati ndani ya siku 14 za kazi).

“Aidha benki itaendelea kutoa elimu ya fedha kwa vikundi na mtu mmoja mmoja kwa gharama zake na kuhakisha inaongeza uchumi shirikishi ili kuongeza kipato cha Mzanzibari mmoja mmoja,” mkurugenzi huyo ameongeza..

Chanzo: www.tanzaniaweb.live