Dar es Salaam. Mkuu wa wilaya ya Kigamboni, Sarah Msafiri, leo Alhamisi Julai 11, 2019, amepokea vitabu 1,500 vya fasihi vilivyotolewa na Benki ya UBA Tanzania kwa shule za sekondari zenye uhitaji zilizopo katika wilaya yake.
Vitabu hivyo vimetolewa na UBA Tanzania kupitia mpango wake wa kuhamasisha usomaji (Read Africa Initiative), sambamba na kutembelea shule za sekondari za Nguva, Aboud Jumbe na Pemba Mnazi, zote zikiwa ndani ya wilaya ya Kigamboni.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Msafiri amesema vitabu hivyo vitasaidia kuwajengea uwezo na ari wanafunzi ya kupenda kujisomea.
Amesisitiza kuwa vitabu hivyo vitasaidia kuongeza idadi ya vyenye ubora kwenye maktaba za shule husika.
“Vitabu hivi vilivyotolewa na benki ya UBA Tanzania, vitasaidia katika kuwajengea vijana wetu kupenda kujisomea na kujiwekea utaratibu wa kujisomea mara kwa mara, pamoja na kuwaongezea uwezo katika masomo yao,” amesema Msafiri.
Kwa upande wake, Mkuu wa kitengo cha biashara ndogo na za kati wa benki hiyo, Geofrey Mtawa amesema vitabu hivyo ni vya hadhi ya juu Afrika na vimeboreshwa zaidi ili kuwawezesha wanafunzi na walimu kuvielewa kwa lugha rahisi na yenye kuelimisha.
Pia Soma
- Meneja tume ya madini mbaroni akituhumiwa kuiba madini
- Muungano wa Tigo na Zantel utakuza uchumi nchini
- TEF waitaka Serikali ya Tanzania kutoa maelezo kuhusu Azory Gwanda
Mbali na kutoa vitabu hivyo, UBA Tanzania imekua ikisaidia sekta ya elimu kwa kutoa vitabu kwenye shule mbalimbali ikiwa ni pamoja na wilaya za Ilala, Temeke, Kisarawe na Pwani, pamoja na kutoa elimu ya ujasiriamali bure kwa vijana na wanawake.