Mwanza. Benki ya Biashara ya DCB imesema itaendelea kushirikiana na manispaa nchini kupitia huduma maalumu kuziwezesha kupata fedha za kutekeleza miradi ya kimkakati. Hayo yalisema jijini Mwanza hivi karibuni na mkurugenzi mtendaji wa DCB, Godfrey Ndalahwa kwenye mkutano wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa (Alat).
Alisema mpango huo utakaosaidia upatikanaji fedha kuendesha miradi ya kimkakati, una masharti wezeshi kwa mkopaji.
“Mchakato wa uanzishwaji wa huduma hii unaendelea, tutakachofanya ni kuongeza manispaa na halmashauri nyingine ambazo pia zina miradi ya kimkakati kuweza kujumuishwa kwenye mpango huu.
“Ombi langu ni kwamba, najua vyanzo viko vingi, lakini hii yenyewe inaweza ikawa chanzo kizuri cha kutafuta fedha na vilevile ni chanzo kizuri kwa ajili ya kusaidia umma wa wawekezaji wakubwa na wadogo kupata fursa ya kuwekeza kwenye miradi yetu,” alisema.
Akizungumza katika Mkutano huo Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alizishukuru taasisi mbalimbali zilizojitokeza kufanikisha Mkutano wa mwaka wa ALAT ikiwemo DCB na kuzitaka zijitokeze Tena mwakani kwa udhamini wao ili kufanikisha mkutano huo.
Mkurugenzi Mtendaji huyo wa DCB alizungumzia pia udhamini na ushiriki wao katika mikutano mbalimbali na shughuli za kijamii ikiwemo Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Shirikisho la Serikali za Mitaa (ALAT) uliofanyika mjini Mwanza hivi karibuni akisema hiyo imetokana na azma ya kuanzishwa kwa benki hiyo ikiwa na kuwahudumia wananchi na wajasiriamali wadogowadogo hasa wanawake na vijana na kufanikiwa kwa azma hiyo kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushirikiano kutoka katika manispaa na halmashari za Jiji la Dar es Salaam ilikoanzishwa.
Pia Soma
- Kim Jong aionya Marekani
- Viongozi Tanzania walivyokibeba Kiswahili SADC
- Serengeti yaandikisha wapiga kura wapya 32,888
Akizungumza mafanikio ya zoezi la uuzaji hisa lililofanyika hivi karibuni Bwana Ndalahwa alisema zoezi hilo lilifanikiwa kwa asilimia 108 na hiyo imechangiwa sana na historia yao na mahusiano yao ya karibu na manispaa na halmashauri kwa maana ya kwamba wao ndiyo waanzilishi.
Kuhusu maendeleo ya DCB na mikakati ya kuzidi kujipanua, Mkurugenzi wa DCB alisema wigo wa kufanya biashara umeongezeka kutoka Dar es Salaam pekee na sasa wameruhusiwa kuendesha biashara nchini nzima wakiwa na matawi manane likiwemo la Dodoma pamoja na mawakala 1000 nchi nzima huku wakipatikana kwenye mtandao hivyo huduma zao kupatikana nchi nzima.
Pamoja na hayo mkurugenzi hiyo alizungumzia huduma yao mpya ya DCB Lamba kwanza inayomwezesha mteja kupata riba ya hadi asilimia 14 siku mteja anapoamua kuwekeza huku akitoa wito kwa watanzania kujiunga na huduma ya DCB Digital kwa njia ya simu za mkononi kwa kubonyeza alama ya nyota 150 nyota 85 reli ili kujiunga na kupata huduma mbalimbali za benki hiyo kwa lugha rahisi wakiita ‘DCB kwanza simu yako Tawi letu’.
Benki ya DCB ilianzishwa mwaka 2002, ikianzishwa na Maspaa za Dar es Salaam na kujulikana kama Benki ya Wananchi wa Dar es Salaam. Lengo kuu ilikuwa ni kusaidia wajasiriamali wadogowadogo. Baada ya kuanzishwa iliweza kutekeleza lengo hilo na na kuendelea kukua. Mwaka 2008 ilikuwa benki ya kwanza kuorodheshwa kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), na iliendelea kukua hivyo hivyo na baadae kubadilisha jina kutoka Dar es Salaam Community Bank na kuwa DCB Commercial Bank kwa sasa.