Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Barrick: Ubia wetu na serikali mfano wa kuigwa

29701bd3939ec23e8bf3f391f5c612ed.png Barrick: Ubia wetu na serikali mfano wa kuigwa

Tue, 23 Feb 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

RAIS na Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Barrick Gold Corp, Dk Mark Bristow amesema ushirikiano kati ya kampuni hiyo na Serikali ya Tanzania ni mfano mzuri wa kuigwa Afrika na duniani.

Aliyasema hayo jana kwenye Mkutano wa Siku Tatu wa Kimataifa wa Uwekezaji katika Sekta ya Madini Tanzania ulioanza juzi na kuhitimishwa leo kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Dk Bristow alisema mwaka mmoja uliopita Serikali ya Tanzania na Kampuni ya Barrick ziliingia mkataba wa ushirikiano ambao umeanza kuzaa matunda ikiwemo serikali kuanza kupata gawio, lakini pia ushirikiano huo unazinufaisha sawa pande zote mbili.

Alisema mkazo uliowekwa na kampuni hiyo kuhusu ubora wa rasilimali madini wanayochimba unawatofautisha na wawekezaji wengi kwenye tasnia ya madini.

“Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza Afrika kuanzisha mkataba bora wa madini mwaka 1997 na kuvutia uwekezaji kwenye sekta ya madini, ushirikiano wetu na serikali ni mzuri na wa kuigwa na tumekuwa mfano Afrika na duniani,” alisema Dk Bristow.

Dk Bristow alisema mipango ya baadaye ya Barrick ni kuendesha shughuli za mgodi wa Bulyanhulu na North Mara kwa pamoja badala ya kila mgodi kuendeshwa peke yake ili kuiingiza Tanzania kuwa nchi ya saba yenye rasilimali ya kundi la kwanza na kuwa na uwezo wa kuzalisha wakia zaidi ya 500,000 kwa mwaka katika miaka 10 ijayo.

Pia alisema mwaka jana Barrick iliwekeza Dola za Marekani milioni 290 kwa ajili ya kuajili wakandarasi na watoa huduma nchini pamoja na kuajiri kampuni za ulinzi za Tanzania, lakini pia walitumia Dola za Marekani milioni 800 kwa ajili ya kulipa kodi, gawio, vibali, uboreshaji wa miundombinu, mishahara na malipo mbalimbali.

Alisema mahusiano ya Barrick na jamii zinazouzunguka yamekuwa bora na kuzidi kuimarika, pia wameimarisha suala la usalama migodini, afya, na utunzaji wa mazingira na kuahidi kuwa ifikapo robo ya ya nne ya mwaka huu, mgodi wa North Mara nao utaingizwa kwenye rekodi ya kimataifa kwa utunzaji wa mazingira.

Naye Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Madini Tanzania (FEMATA), John Bina alisema Tanzania ina aina zaidi ya 260 za madini ambayo ni fursa kwa Watanzania wanaotaka kuwekeza kwenye sekta hiyo.

Bina aliwataka vijana wa Kitanzania wanaomaliza vyuo vikuu kujikita kwenye sekta ya madini badala ya kusubiri kuajiriwa kwani madini ni ajira ya uhakika.

Makamu Rais wa Kampuni ya Dhahabu ya Geita (GGM), Simon Shayo alisema mipango yao ni kuhakikisha GGM inakuwa mchangiaji mkubwa wa asilimia 10 ya Pato la Taifa iliyowekwa kwenye sekta ya madini ifikapo mwaka 2025.

Kuhusu tuzo tatu walizopata jana, alisema zimetokana na ushirikiano mzuri walionao na serikali na wadau, lakini pia uwekezaji wa kweli unaogusa maisha ya watu na siyo tu suala la kuweka fedha na kupata faida.

Chanzo: habarileo.co.tz