Dar es Salaam. Balozi wa zamani wa Tanzania nchini Afrika Kusini, Ami Mpungwe amesema Tanzania inahitaji kuwa na sera na mikakati inayoendana na wakati uliopo ili kufikia uchumi wa viwanda.
Akizungumza leo usiku Alhamisi Oktoba 4, 2018 katika mjadala wa Jukwaa la Fikra la Mwananchi, Balozi Mpungwe amesema Tanzania lazima iwe na mfumo wa uchumi unaoendeshwa kwa ushindani.
Amesema Tanzania ina fursa nyingi lakini ukuaji uchumi wake hauendani sawia.
"Tanzania kuna pamba ya kutosha lakini nguo zinazotengenezwa zinaweza kushindana kidunia? Lazima kuwe na sera itakayowezesha," amesema.
Amesema ili kufikia uchumi wa viwanda, Tanzania inahitaji tafakari ya ndani na kina. Pia, kuimarisha sera itakayowezesha ushindani wa bidhaa zinazozalishwa.
Balozi Mpungwe amesema nchi ina nafasi ya kuwekeza katika Soko la Pamoja la Afrika Mashariki kama fursa nyingine kupitia viwanda.
Pia, Balozi huyo amesisitiza ujenzi wa viwanda vya madini vitakavyoleta ushindani wa kidunia kupitia bidhaa zitakazozalishwa.