Tabora. Waziri wa Kilimo, Japhet Hasunga ameitaka Bodi ya Tumbaku Tanzania kuhakikisha tumbaku yote itakayovunwa msimu huu inanunuliwa bila visingizio.
Ametoa agizo hilo leo Alhamisi Januari 17, 2019 wakati akifungua mkutano wa mwaka wa wadau wa tumbaku nchini.
Amebainisha kuwa kumekuwa na changamoto ya kununua tumbaku msimu uliopita, kusisitiza kuwa hataki itokee tena msimu huu.
Katika kusaidia kupatikana kwa masoko, Hasunga amesema wizara yake imeanzisha kitengo cha masoko kwa sababu hawajaridhika na wanunuzi waliopo.
Amesisitiza kwamba wanataka ongezeko la wanunuzi kwa lengo la kuongeza ushindani na kufanya bei kuongezeka.
Tani 54,800 za tumbaku zinatarajiwa kuvunwa na wakulima wa Mkoa wa Tabora.