Dar es Salaam. Rais John Magufuli ameipongeza Wizara ya Kilimo kwa kazi nzuri hususani ununuzi wa korosho za wakulima huku akisema kuna akaunti 3,000 za wanunuzi wasio na mashamba maarufu kama ‘kangomba’ zimefungiwa.
Akizungumza leo Ijumaa Januari 4, 2019 katika utiaji saini wa mkataba wa ununuzi wa tani 36,000 za mahindi kati ya Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP) na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA).
“Ninajua hata ununuzi wa korosho unakwenda vizuri. Najua wanaopiga piga kelele ni wale makangomba walinunua korosho wakifikiri watapewa hela wakiulizwa mashamba yako wapi hawayaonyeshi, kwa hiyo hawalipwi,” amesema.
“Tumeshajua kuna akaunti zingine feki karibu 3,000 za watu walizokuwa wamefungua, hazifanyi kazi, si ndiyo bwana kaka?”
Ameongeza, “Kwa hiyo sisi tunaendelea ku deal (kushughulika) na hivyo. Ukitaka kufanya biashara ufanye biashara takatifu, ukitaka kupata hela ufanye biashara nzuri kama ya Michael (Dunford) pamoja na WFP ambayo haina mashaka yoyote.”
Amewataka wafanyabiashara kuwa waaminifu na kufanya kazi bila kujificha.