Kiwanda cha kuzalisha Sukari cha Mkulazi kilichopo Wilayani Kilosa mkoani Morogoro, kinatarajiwa kuzalisha ajira za moja kwa moja na muda mfupi kwa vijana zaidi ya 5,000 nchini.
Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini Mfuko wa Hifadhi wa Jamii (NSSF), Mwamini Juma Malemi leo Desemba 22, 2023 baada ya kutembelea na kukagua kiwanda hicho, ambacho hadi sasa kimekamilika kwa asilimia 100 na tayari kimeanza kazi.
Malemi amesema, ajira hizo zitasaidia kuondoka wimbi la vijana waliokosa ajira kwa muda mrefu.
"Ajira bado zinahitajika, lakini kwa hatua ya kukamilika kwa kiwanda hiki kumeonyesha nafuu kwa vijana wetu kupata kazi na kuacha kuwa tegemezi kwa familia na jamii kwa ujumla," amesema.
Aidha amesema kuwa sukari inayozalishwa katika kiwanda hicho itaanza kupatikana madukani hivi karibuni.
“Tumejipanga pia kuwa na duka maalumu litakalouza sukari kwa bei elekezi ya kiwanda,”amesema.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa bodi ya Mkulazi, Dk Heridelita Msita amesema kuwa kiwanda hicho kimeanza kazi na kuwahakikishia Watanzania upatikanaji wa sukari ya kutosha.
Dk Msita amesema kuwa hadi sasa baadhi ya kampuni zimeweka oda ya kupata sukari inayozalishwa katika kiwanda hicho, ambacho kimekuwa na manufaaa kwa wananchi na vijana kwa kupata ajira na kujiongezea kipato chao.