HOTELI ya Serena na Hospitali ya Agha Khan nchini Tanzania, zimeonesha nia ya kutaka kuwekeza katika Hifadhi ya Msitu Asilia wa Amani.
Hayo yalibainika katika kikao baina ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro na wawakilishi wa Hoteli ya Serena na Hospitali ya Agha Khan kilichofanyika jana jijijini Dar es Salaam.
Katika kikao hicho, Dk Ndumbaro aliwaeleza wawakilishi hao kuwa Hifadhi ya Msitu Asilia wa Amani iliyopo mkoani Tanga ni sehemu nzuri ya kiutalii inayohitaji wawekezaji kwa ajili ya ujenzi wa hoteli za kitalii.
Alisema Kampuni ya Serena imekuwa ikifanya vizuri katika hoteli, hivyo ni muhimu kwayo kuchangamkia fursa hiyo ya kuwekeza katika msitu huo kwa vile ni eneo lenye vivutio lukuki vya utalii na vinavyoweza kuipa tija ndani ya muda mfupi.
Mbali na msitu huo, Dk Ndumbaro aliziitaja fursa nyingine muhimu kwa wawekezaji hao kuwekeza nchini kuwa ni pamoja na katika Msitu Asilia wa Kazimzumbwi ulipo mkoani Pwani, Maporomoko ya Kalambo, Msitu wa Maghamba pamoja na Hifadhi ya Msitu Asilia wa Rungwe uliopo mkoani Mbeya ili kukuza utalii wa ikolojia ambao utalii a unaopendwa na watu wengi wa ndani na nje ya nchi.
Katika hatua nyingine, Mwakilishi wa Hospitali ya Agha Khan, Sisawo Kontech amemweleza Waziri wa Maliasili na Utalii kuwa kampuni hiyo imeanza kujenga hospitali katika Jiji la Mwanza ili kutoa huduma kwa jamii pamoja na kukuza utalii wa matibabu.
Alisema kupitia Hospitali za Agha Khan, wamedhamiria kukuza utalii wa matibabu nchini ili kuvutia watalii kutoka nchi mbalimbali kuja ya kupata huduma katika hospitali hizo.
Mintarafu utalii huo, Waziri Ndumbaro alisema serikali ipo tayari na itatoa ushirikiano kwa ajili ya kukuza aina hiyo ya utalii nchini.