NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Atupele Mwakibete ameitaka idara ya Masoko ya Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL) kufanya tafiti na kuja na mpango madhubuti wa bei za tiketi ili kuruhusu abiria wengi zaidi kutumia usafiri huo.
Akizungumza na Menejimenti ya ATCL Naibu Waziri Mwakibete amesema Serikali imewekeza fedha nyingi na inategemea shirika hilo kupata faida hivyo uwepo wa nauli zinazohimilika kutaongeza idadi ya abiria, pato na hatimaye shirika kuendelea kukua.
“Shirika hili limewekezwa fedha na idara kuu ambayo inaweza kufanya shirika hili kuendelea kibiashara ni idara ya masoko hivyo,mjipange vizuri ili kulifanya shirika kupata faida na kuweza kujiendesha’ amesema Mwakibete.
Aidha, Mwakibete amesema ni wakati sasa wa ATCL kuboresha kitengo cha huduma kwa wateja kwa kuhakikisha kama kuna taarifa za kuahirishwa kwa ndege abiria wanapewa taarifa mapema na kwa utaratibu unaoeleweka.