MABONDIA kutoka nchi tano watapanda ulingoni Mei 28 katika pambano lililopewa jina la Rhumble in Dar 2 kwenye ukumbi wa Next Door Arena, Oyesterbay.
Mabondia hao na nchi zao kwenye mabano ni Brendon Denes (Zimbabwe), Sibusiso Zingange (Afrika Kusini) Olanrewaju Durodora (Nigeria) na Chris Thompson ambaye naye anatoka Afrika Kusini.
Kwenye orodha hiyo pia wapo Ardi Ndembo anayetoka Congo Brazaville, Simon Madhanire (Zimbabwe) na mabondia wawili kutoka Bulgaria, Pench Tsvetkov na bondia nyota wa kike, Joana Nwamerue.
Wakati Denes atazichapa na bondia nyota wa Tanzania, Hassan Mwakinyo kuwania ubingwa wa Afrika (ABU) wa uzito wa Superwelter, Zingange atashuka ulingoni kuzichapa na bondia Ibrahim Class katika pambano la Light.
Bondia Durodora atapmabana na nyota mwingine wa Tanzania, Shaban Jongo katika uzito wa Cruiser wakati bondia mkali wa uzito wa juu wa Congo Brazzavile, Ndembo atazichapa na Simon Madhanire wa Zimbabwe.
Pia kutakuwa na mapambano yanayowahusisha mabondia Thompson ( Afrika Kusini), Joana Nwamerue (Bulgaria) na Pencho Tsvetkov pia wa Bulgaria katika usiku huo ambao umedhaminiwa na Benki ya KCB, Bodi ya Utalii, DStv, Onomo Hotel, M- Bet, Plus Networks Limited.
Pambano hilo limeabdaliwa na Kampuni ya Jackson Group Sports kwa kushirikiana na Global Boxing Stars na Epic Sports and Entertainment.
Ofisa Mtendaji Mkuu wa Jackson Group Sports, Kelvin Twissa amesema kuwa mabondia wote wapo katika mazoezi makali kuelekea siku hiyo.