Michezo

Habari

Burudani

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kidunda aitaka mikanda ya dunia

Selemani Kidunda Bondia kutoka Jeshi la Wananchi Tanzania, Selemani Kidunda

Thu, 19 Aug 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

Bondia wa ngumi za kulipwa, Selemani Kidunda amesema kitu kitakachomfanya ajivunie kazi hiyo ni kupambana kupata mikanda ya kimataifa.

Akizungumza Dar es Salaam jana, bondia huyo alisema anatamani siku moja awe mshindi wa mikanda ya dunia ya WBC, WBO na WBA na ili kufikia kiwango kikubwa anaendelea na mazoezi akiamini ipo siku ndoto yake itatimia.

“Naamini Mwenyezi Mungu atanijalia kufika ninapopataka, nijitahidi nifanye vizuri katika mapambano yangu yote nipate mikanda mikubwa itakayoacha alama katika kazi yangu,” amesema.

Kidunda aliyewahi kuitumikia timu ya taifa ya ngumi za ridhaa kwenye mashindano mbalimbali ya kimataifa, alisema namna ambavyo kiwango chake kinakua inampa faraja na kujiamini kuwa atafika pale anapotaka.

Bondia huyo tangu amejiunga na ngumi za kulipwa amecheza mapambano matano na yote ameshinda kwa ‘knockout.’

Ubora wa kiwango chake katika uzito wa Super Middle umemfanya kupanda, ambapo kwa mujibu wa takwimu za Boxrec, anashika nafasi ya tatu Tanzania kati ya mabondia 14 na nafasi ya 271 duniani kati ya mabondia 1,166.

Alisema namna anavyokuja kwa kasi, baadhi ya mabondia wamekuwa wakimuogopa kupambana naye.

Kesho atakuwa ni miongoni mwa mabondia watakaopanda ulingoni kuchuana na Constantino Bonabucha kwa ajili ya kusindikiza pambano kuu la Abdallah Pazi ‘Dulla Mbabe’ dhidi ya Twaha Kiduku litakalopigwa Ubungo, Dar es Salaam.

Chanzo: www.habarileo.co.tz