BONDIA wa Tanzania, Twaha Kiduku (pichani) amempiga bondia Tshibangu ‘Beberiko’ Kayembe wa Jamhuri ya Kidemokrasia Congo katika pambano lililochezwa jijini Dar es Salaam juzi.
Wababe hao walikutana kwenye pambano lisilo na ubingwa la raundi nane lililovuta idadi kubwa ya mashabiki na kuoneshwa mubashara na kituo cha televisheni cha Azam.
Majaji watatu wa pambano hilo wote walimpa ushindi Kiduku, katika raundi sita kati ya raundi nane za pambano hilo.
Kiduku alionekana akiwa tofauti katika pambano hilo, akiwa ametulia na kupiga kwa kutafuta pointi za ushindi zaidi kuliko mtindo wake uliozoeleka wa kutumia nguvu zaidi.
Tshibangu ambaye aliwahi kupigana na bondia Hassan Mwakinyo na kupoteza pambano hilo, juzi alikuwa mgumu dhidi ya Kiduku kwa kuonesha uwezo wa kuvumilia masumbwi mazito.
“Pambano lilikuwa zuri, namshukuru Mungu kwa sababu mpinzani wangu naye alijiandaa. Hizi ni ngumi huwezi kulazimisha kupata KO, nilijaribu lakini KO inakuja yenyewe wakati wa mchezo ukiilazimisha utapata madhara,” alisema Kiduku.
Kiduku alisema tayari amesaini mkataba wa kupigana tena na Dullah Mbabe Juni 26, ambapo katika pambano lao kwanza lililofanyika mwaka jana, Kiduku alishinda kwa pointi.
Kwa upande wa Tshibangu, alisema ameridhika na uamuzi wa majaji wa pambano hilo na anajipanga kurejea tena ulingoni.