Hatimaye bondia namba mbili nchini kwenye uzani wa super middle, Abdallah Pazi ‘Dullah Mbabe’ amehitimisha safari yake ya mapumziko ya muda aliyojiwekea na sasa amerejea rasmi kwenye ndondi.
Mbabe aliamua kujipa mapumziko hayo siku chache baada ya kuchapwa nyumbani na Tshimanga Katompa wa DR Congo, pambano lililokuwa gumzo nchini na Mbabe kuliambia gazeti hili kuwa ameamua kupumzika ndondi kwa muda mrefu.
Tangu Oktoba alipochapwa, bondia huyo hakuwahi kuonekana ulingoni hadi juzi alipoliambia gazeti hili kuwa anarudi upya.
“Nimemaliza kipindi kirefu cha mapumziko nilichojiwekea, sasa kazi zije tu, niko fiti na yeyote atakayejipendekeza ni halali yangu,” alitamba Mbabe juzi akiwa mazoezini.
Alisema ameanza ratiba ya mazoezi jijini Dar es Salaam, tayari kupanda ulingoni.
“Narudi upya, kama nilivyosema ikitokea pambano ambalo nitaona linaendana na mimi nacheza, mashabiki wangu wakae mkao wa kuona kazi za bondia wao,” alisema.
Mbabe aliamua kupumzika baada ya kupigwa mfululizo, kabla ya kuchapwa na Katompa alitoka kuchezea kipigo cha Twaha ‘Kiduku’ Kassim bondia namba moja kwenye uzani wa super middle na mpinzani wake ulingoni.
Vipigo hivyo vilizua utani mwingi kwenye mitandao.