BONDIA wa uzito wa Super Middle, Abdallah Pazi ‘Dulla Mbabe’ amesema maandalizi ya pambano lake dhidi ya Alex Kabangu kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) yamekamilika na kuwaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi kumpa sapoti.
Dulla Mbabe atapambana na Kabangu mwenye rekodi ya kucheza mapambano 10 kati ya hayo ameshinda matano, amepoteza matatu na kutoka sare mara mbili jambo linaloonesha kuwa sio bondia wa kubezwa.
Mara ya mwisho kupoteza pambano ilikuwa mwaka 2020 alipopigwa na Ryno Liebenberg.
Pambano hilo ambalo litapigwa Jumamosi ijayo, awali lilipangwa kufanyika Mei 28, mwaka huu katika viwanja vya PTA, Sabasaba, Dar es Salaam.
Akizungumza na gazet hili, Dulla Mbabe alisema anajua kiu ya mashabiki wake ni kuona anaibuka na ushindi katika pambano lijalo ili kurejesha imani baada ya kupoteza dhidi ya Twaha Kiduku.
“Najua mashabiki wangu hawataki kuona kile kilichotokea katika mchezo uliopita, nawaahidi kuwa pambano hili litakuwa ni salamu kwa mabondia wanaotamani kupanda ulingoni na mimi,” alisema Dulla Mbabe.