BAADA ya kumtwanga Mkenya, Daniel Wanyonyi, bondia Mtanzania, Abdallah Pazi 'Dula Mbabe' amewatahadharisha mabondia wa ndani na nje ambao wana mpango wa kupigana naye kujiandaa na kifo.
Bingwa huyo wa zamani wa Dunia wa WBO, amesema tangu kupoteza pambano lake dhidi ya Twaha Kiduku amebadilika na kikubwa ambacho amekusudia ni kurudisha heshima aliyokuwa nayo kwenye mchezo huo.
“Ukweli nimepania kufanya kitu ambacho kitaweka historia kwenye mchezo wa ngumi Tanzania ndio maana mapambano yangu mawili yaliyopita nimeshinda ndani ya raundi ya kwanza na hii ni onyo kwa mabodia wa ndani na nje yeyote anayetaka kupanda ulingoni na mimi ajiandae na kifo,” alisema Dula Mbabe.
Bondia huyo alisema baada ya pambano lake dhidi ya Wanyonyi, anarudi Gym kuendelea na mazoezi akisubiri mpinzani kutoka kokote duniani ikiwamo pambano lake la marudiano dhidi ya mpinzani wake, Twaha Kiduku.
Alisema anahamu kubwa ya kurudiana na Kiduku ili kukata mzizi wa fitina ambao umekuwa ukimuumiza kwa muda mrefu baada ya kupoteza pambano mwaka jana.
Dula Mbabe alisema pamoja na mpinzani wake kumuhitaji bondia namba moja nchini Hassan Mwakinyo, lakini angeomba wamalize kwanza hicho kiporo kwa kurudiana ili ajulikane mbabe wa jumla kati yao ni nani.
Dullah Mbabe alitumia sekunde tano kumtwanga kwa KO Wanyonyi katika pambano lililofanyika Ijumaa iliyopita jijini Dodoma.