LIGI ya Kikapu Mkoa wa Dar es Salaam imenoga baada ya timu nne za wanaume kuingia nusu fainali kwa ajili ya kutafuta bingwa wa kuwakilisha michuano ya taifa.
Timu zilizotinga hatua hiyo ni ABC, JKT, Oilers na Kurasini Heat na sasa zinatarajiwa kuchuana kesho kusaka tiketi ya fainali. ABC ilitinga hatua hiyo baada ya kuiondosha VBC katika mchezo wa hatua ya mtoano ambapo kati ya michezo mitatu ilishinda miwili na kufungwa mmoja.
Mchezo wa kwanza walifungwa 71-81, wa pili walishinda 81-71 ikalazimika wacheze mchezo wa tatu kutafuta mshindi na ndipo ABC wakashinda kwa vikapu 80-75.
Kwa upande wa JKT ilishinda michezo miwili dhidi ya Ukonga Kings vikapu 85-65, 68-60, Oilers ikishinda dhidi ya Pazi vikapu 80-70, 71-58 na Kurasini Heat ikishinda 58-51, 90-58.
Kwa matokeo hayo, nusu fainali ya kwanza itachezwa kesho kati ya JKT dhidi ya Oilers na ya pili itachezwa keshokutwa kati ya ABC dhidi ya Kurasini heat.