Mwanamuziki kutoka Jamhuri ya Kongo, Ferre Gola na msanii wa Bongo Fleva nchini Tanzania, Yusufu Mbwana 'Mbosso' watatumbuiza kusindikiza usiku wa mashindano Miss East Africa.
Hayo yamesemwa leo Jumanne Desemba 14, 2021 na Mritibu wa mashindano hayo, Hellen Kazimoto katika mkutano na waandishi wa habari kuhusu mashindano hayo ambayo yanatarajiwa kufanyika Desemba 24 ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Kazimoto amesema mbali na warembo kupita jukwaani siku hiyo, kutakuwepo na burudani na kuwataja wasanii hao kuwa ndio watalipamba shindano hilo.
Kwa upande wake Makamu wa Rais wa kampuni ya Rena ambao ndio waandaaji wa mashindano hayo, Jolly Mutesa amesema washiriki kutoka nchi 14 zitashiriki na kuzitaja kuwa ni pamoja na Moritius, Sudani ya Kusini,Djbout, Elitrea, Shelisheli,Comoro, na Uganda.
Nchi nyingine ni Kenya, Uganda, Malawi, Somalia, Ethiopia, Burundi, Ruanda, Malawi na wenyeji Tanzania.
Advertisement Jolly amesema mshindi katika mashindano hayo atapata zawadi ya gari aina ya Nissan Xtrail na mshahara wa mwezi mmoja wa dola 1500, wakati mshindi wa pili ataondoka na na kitita cha dola 5000 huku mshindi wa tatu atapata dola 2000.
Akizungumza kama mdhamini mkuu wa shindano hilo, kutoka kampuni ya Wasafi, Jamal April amesema katika mashindano hayo warembo wanaangaliwa katika mambo mbalimbali na sio uzuri tu wa sura na umbo, bali kujiamini, namna ya kuweza kutangaza nchi zao na Bara la Afrika kwa ujumla na kufanya programu mbalimbali za kusaidia jamii.