Mkali wa wimbo wa Chafu Pozi,Billnass amemvalisha pete ya uchumba msanii wa Bongo Fleva Faustina Charles maarufu Nandy.
Nandy na Billnass waliwahi kuwa wapenzi miaka ya nyuma na mahusiano yalikatika na baadaye Nady kuwa na uhusiano na marehemu Ruge Mutahaba mpaka pale umauti ulipomkuta.
Hata hivyo miezi michache baada ya Ruge kufariki wawili hao wamekuwa wakionekana mara kwa mara maeneo mbalimbali lakini kila walipoulizwa kama wamerudiana walikanusha jambo hilo.
Jambo hilo lilisahaulika hasa pale walipoachia wimbo wao wa 'Bugana' na watu kufikiri kwamba wapo kikazi kama ambavyo mara nyingi na wao wamekuwa wakijibu wanapohojiwa na pia kuitana kaka na dada.
Wahenga wanasema penzi ni kikohozi kulificha huliwezi, ambapo jana usiku Aprili 10, 2020 Bilnass alifika ghafla katika shoo ya mtandaoni ya Nandy inayoandaliwa na TVE na kumvisha mkali huyo wa wimbo wa Ninogeshe pete ya uchumba.
Billnass aliyekuwa amevalia koti leusi lenye vimetometo na suruali nyeupe, alifanya kitendo hicho Nandy alipokuwa akiimba wimbo wake wa 'Labda nizikwe' ambapo alipanda jukwaani na kufanikisha jambo lake hilo.
Pia Soma
- VIDEO: Ali Kiba aeleza sababu kupanda, kushuka wimbo Dodo Youtube
- Wimbo Dodo wazua jambo Youtube, meneja wa Ali Kiba azungumza
- Msanii mpya WCB huyu hapa
Kabla ya kumvalisha Nandy pete,Billnas alipiga magoti jambo lilionyesha Nandy kitoamini anachokiona mbele ya macho yake na machozi kuonekana kumlenga huku akiwa ameshika kipaza sauti.
Billnass ambaye jina lake halisi ni Willium Lyimo, alimwambia mrembo huyo kuwa "Leo ni siku yangu ya kuzaliwa naamini tumekuwa pamoja muda mrefu,tumepitia vitu vingi vizuri na vibaya najua upande wako mzuri na upande wako mbaya nimechagua vyote,natamani dunia nzima ijue nakupenda, Nakupenda',amesema Billnass.
Msanii huyu hakuishia hapo kwani mara baada ya kumaliza kumvalisha Nandy pete hiyo alimwambia "Katika maisha yangu sijawahi kufanya kitu kikubwa kama hiki kwa hiyo leo ni siku muhimu sana ni siku ya kipekee
" Naamini ndio mwanzo wa ukurasa mwingine wa maisha yangu kwa hiyo ambacho naweza kukuambia nazidi kukuombea usiwe mzuri tu kwangu bali na kwa mama wa watoto wangu,"amesema Billnass na kisha kumwimbia wimbo wa rap wenye mashairi ya mapenzi.