Mhariri Mwandamizi wa BAKITA, Oni Sigalla, amesema baadhi ya wasanii wa muziki wa kizazi kipya hawana Benki iliyojaa misamiati mingi ya kuwasaidia katika nyimbo zao badala yake wanatumia lugha za matusi, ambazo si rahisi kuzisikiliza ukiwa na watu unaowaheshimu.
Kauli hiyo ameitoa leo Agosti 20, 2021, kwenye mjadala uliohoji iwapo jamii inaridhishwa na maudhui ya muziki wa kizazi kipya, ulioendeshwa na kipindi cha Supa Breakfast cha East Africa Radio.
"Leo hii vijana wetu (Wasanii) mniwie radhi, sasa wamekuwa na Benki ndogo sana ya misamiati, hana mbadala wala uwezo wa kufikiria kwamba hili ninaweza kuzunguka kona hii nikaamaanisha hivi wao wanaenda na njia ya mkato moja kwa moja," amesema Oni Sigalla
Aidha, ameongeza kuwa, "Uwezo wa mtu kuzungumza ndiyo ukomo wa akili yake, tunadhani wasanii wetu baadhi wamefikia mahali ambapo wanadhani muziki ni sehemu pekee ambako anaweza kujimwayamwaya na matusi na anaweza kuzungumzia jambo lolote baya".