Makanisa nchini Zambia yameagizwa kupunguza muda wa ibada hadi saa mbili kama sehemu ya hatua za kuzuia kuenea kwa ugonjwa wa kipindupindu.
Hakuna uuzaji wa vyakula vinavyoharibika na vilivyo tayari kuliwa katika makanisa yote, Ndiwa Mutelo, afisa mkuu anayehusika na masuala ya kidini, alisema.
Waumini pia wametakiwa kuepuka kusalimiana kwa mikono na kukumbatiana ili kupunguza hatari ya kuambukizwa ugonjwa huo.
Bw Mutelo katika taarifa pia aliagiza vituo vya ibada kuwapa washiriki wao maji salama ya kunywa, sehemu za kunawia mikono pamoja na dawa za kujisafisha mikono.
Zaidi ya visa 7,800 vya kipindupindu vimeripotiwa nchini kote tangu Oktoba mwaka jana.
Katika saa 24 zilizopita, kulikuwa na visa vipya zaidi ya 400 na vifo 18, wizara ya afya ilisema.