Miongoni mwa zaidi ya watu 100 waliozama mapema wiki hii wakati mashua ilipopinduka kwenye Mto Niger katikati mwa Nigeria walikuwa wazazi wengi waliokuwa wakijaribu kuwaokoa watoto wao, mtu aliyenusurika aliambia BBC.
Mohammed Alhassan, mwenye umri wa miaka 22, alikuwa mmoja wa watu wapatao 300 waliokuwa wakisafiri kwa boti ya mbao iliyojaa watu wengi huko Patigi katika Jimbo la Kwara.
Wengi walikuwa wakirudi kutoka kwenye harusi. Lakini si Bw Alhassan - alikuwa anarudi kutoka sokoni.
Haonyeshi hisia zozote anaporudi kwenye ukingo wa mto ambako alikuwa amefanikiwa kuogelea hadi salama.
Lakini anapokumbuka wazazi waliozama na watoto wao, akiwemo dada yake na mtoto wake wa kiume mwenye umri wa miaka minane, machozi yanamtoka.
"Wanawake walibaki nyuma wakijaribu kubeba watoto wao - baadhi yao walikuwa na watoto watatu au wanne.
"Pia kulikuwa na baba ambao walikufa kwa njia hiyo hiyo wakijaribu kuokoa watoto wao," anasema.
Angejaribu kusaidia kuwaokoa pia, angezama, anasema.
Kwa hiyo aliogelea hadi mahali usalama, lakini alipofanya hivyo, aliona hali ya kutisha wakati akina mama na baba wakizama pamoja na watoto wao walipokuwa wakijaribu kuwaokoa.