Waziri wa Ulinzi wa Liberia Prince Charles Johnson III amejiuzulu kufuatia maandamano ya wake za wanajeshi wa nchi hiyo wanaomlaumu kwa ujira mdogo na hali mbaya ya maisha katika kambi za kijeshi.
Wanawake hao waliweka vizuizi karibu na mji mkuu, Monrovia na kwingineko nchini, na kumlazimisha Rais Joseph Boakai kufuta sherehe za Siku ya Jeshi la Kitaifa mnamo Jumatatu.
Walimtaka waziri wa ulinzi ajiuzulu, wakimlaumu kwa kupunguzwa kwa mishahara ya wanajeshi wa Liberia wanaorejea kutoka misheni ya amani nchini Mali.Wenzi wa maafisa hao pia walikashifu ukosefu wa usalama wa kijamii, uhaba wa umeme na ufisadi ndani ya jeshi.
Maandamano hayo yalianza siku ya Jumapili karibu na kambi ya Edward Binyah Kesselly, mjini Monrovia.
Bw Johnson, katika taarifa, anasema anajiuzulu kutokana na "vurugu za kisiasa na za kiraia" zinazosababishwa na maandamano hayo.
Hata hivyo alikanusha madai ya matumizi mabaya ya fedha jeshini na kuongeza kuwa matakwa yake ni kuhakikisha nidhamu inawekwa katika jeshi hilo.
Rais Boakai, ambaye aliapishwa Januari, kupitia ofisi yake alisema malalamishi ya wanawake hao yatachunguzwa na kushughulikiwa.